Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Niwasaidie Wengine?

Kwa Nini Niwasaidie Wengine?

 Siri mbili ambazo watu wengi hawajui

 Siri ya #1: Unapotoa, huenda utapata pia!

 Watu watatambua kwamba wewe ni mkarimu. Kwa sababu hiyo, huenda watakuonyesha ukarimu. Biblia inasema hivi:

  •  “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. . . . Kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”​—Luka 6:​38.

  •  Siri ya #2: Unapowasaidia wengine, unajisaidia!

     Kuwatendea wengine mema kunakufanya ujiheshimu na kunakufanya upate uradhi unaotokana na kutoa. Biblia inasema hivi:

  •  “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

  •  “Unapoandaa karamu, alika maskini, viwete, vilema, vipofu; nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hao hawana kitu cha kukulipa.”​—Luka 14:13, 14.

Vijana wanaojali

  Kila mahali kuna vijana wanaowajali watu wengine! Ifuatayo ni mifano kadhaa.

 “Nyakati nyingine ninapotaka kuketi tu na kutazama televisheni, mimi hufikiria kuwahusu Mama na Baba, wakiwa kazini, na jinsi watakavyokuwa wamechoka watakaporudi nyumbani. Kwa hiyo, mimi huinuka na kuosha vyombo na nyumba. Pia mimi huwatayarishia kahawa kwa sababu wazazi wangu wanapenda kahawa. Mama anaporudi nyumbani, yeye husema, ‘Ala, nyumba ni safi! Na inanukia vizuri. Asante sana, Mpenzi!’ Mimi hufurahi sana ninapowafanyia Mama na Baba jambo fulani zuri kama hilo.”​—Casey.

 “Sikuzote wazazi wangu wamenitegemeza, wameniandalia kila kitu ninachohitaji. Kwa hiyo, gari lao lilipopatwa na shida kubwa mwaka uliopita, nililipa ili lirekebishwe, hata ingawa nililazimika kutumia kiasi kikubwa cha pesa nilizokuwa nimeweka akiba. Bila shaka, wazazi walijaribu kunizuia nisifanye hivyo, lakini nilisisitiza. Wazazi wangu wanastahili mengi zaidi kuliko kile nilichowafanyia. Lakini nilijihisi vizuri sana kuwaonyesha ukarimu na kuwapa kitu fulani.”​—Holly.

 Je, wajua? Vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova wamefurahia kuwasaidia watu kupitia kazi yao ya kufundisha Biblia. Wengine wamehamia nchi nyingine ambako kuna uhitaji mkubwa wa walimu wa Biblia.

 “Nilitoka Marekani na kuhamia Mexico ili kusaidia kuwafundisha watu Biblia. Nyakati nyingine ni vigumu kuwaonyesha wengine ukarimu kwa kuwapa pesa au vitu vingine kwa sababu sina vitu vingi vya kutoa. Lakini nimegundua kwamba ninapotumia wakati na nguvu zangu katika huduma, watu wanathamini hilo kuliko kuwapa vitu vya kimwili.”​—Evan.

Ninaweza kuwasaidiaje wengine?

  Je, ungependa kupata shangwe inayotokana na kuwasaidia wengine? Yafuatayo ni mapendekezo kadhaa.

 Kuisaidia familia yako:

  •  Safisha nyumba, osha vyombo, au usafishe chumba chako​—bila kuombwa ufanye hivyo

  •  Pika

  •  Waandikie wazazi wako kadi ya kuwashukuru

  •  Msaidie ndugu au dada yako kufanya kazi alizopewa shuleni

 Kuwasaidia watu ambao si wa familia:

  •  Mtumie kadi mtu ambaye hajisikii vizuri

  •  Msaidie jirani mwenye umri mkubwa kusafisha uwanja ulio nje ya nyumba yake

  •  Mtembelee mtu ambaye hawezi kutoka nyumbani kwa sababu ya ulemavu

  •  Mnunulie zawadi mtu anayekabili hali ngumu

 Pendekezo: Tafuta jambo ambalo halijatajwa unaloweza kufanya. Kisha azimia kumsaidia mtu mmoja juma hili. Utashangaa kwamba utajihisi vizuri sana.

 “Unapowasaidia wengine, wewe mwenyewe unafurahi. Unahisi kwamba ulitimiza jambo fulani, na unaona kwamba wengine walithamini sana ulichofanya. Unaweza pia kufurahia kulifanya​—hata ingawa mwanzoni hukufikiria kwamba ungefurahia. Huenda baadaye usihisi kana kwamba ulijidhabihu, kwa sababu unapata shangwe kubwa baadaye.”​—Alana.