Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Niongeze Idadi ya Marafiki Wangu?

Je, Niongeze Idadi ya Marafiki Wangu?

 “Mimi hujihisi huru zaidi ninapokuwa na kikundi kilekile cha marafiki, na si rahisi kwangu kutafuta marafiki wengine wapya.”​—Alan.

 “Nina marafiki wachache, na nisingependa sana kutafuta wengine. Si kawaida kwangu kuwafikia watu nisiowajua na kuzungumza nao.”​—Sara.

 Je, una hisia kama za Alan na Sara? Je, una kikundi cha marafiki wa karibu sana na unahisi si rahisi kutafuta marafiki wengine wapya?

 Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia!

 Matatizo ya vikundi vya marafiki

 Hakuna ubaya wa kuwa na kikundi cha marafiki wa karibu. Kuwa na kikundi cha marafiki wa karibu kunakufanya ujihisi una thamani na kwamba unakubalika, licha ya mapungufu yako na mambo mengine.

 “Mtu hufurahi kupendwa na wengine na kuwa sehemu ya kikundi fulani. Unapokuwa kijana ungependa ukubaliwe na vijana wengine.”​—Karen, 19.

 Je, Wajua? Mitume 12 wa Yesu walikuwa miongoni mwa marafiki wengi wa Yesu lakini mitume watatu kati ya hao​—Petro, Yakobo, na Yohana​—ndio waliokuwa marafiki wake wa karibu sana.​—Marko 9:2; Luka 8:​51.

 Hata hivyo, kushirikiana na kikundi fulani tu cha watu na kuwatenga wengine, kunaweza kuleta matatizo. Kwa mfano:

  •   Kutakuzuia kuanzisha urafiki mwingine mzuri.

     “Kuwa na marafiki wanaofanana nawe kutakufanya ukose mambo mapya na usifahamiane na watu wazuri sana.”​—Evan, 21.

  •   Kunaweza kufanya uonekane kuwa mtu mwenye dharau.

     “Unapokuwa na kikundi fulani cha marafiki, unaweza kuonyesha kwamba hutaki kuzungumza na mtu mwingine yeyote.”​—Sara, 17.

  •   Kunaweza kukufanya ushiriki kuwaonea wengine.

     “Huenda mtu asiwe na kawaida ya kuwaonea wengine, lakini ikiwa rafiki zake wanafanya hivyo, hatimaye anaweza kuliona jambo hilo kuwa sawa na lenye kufurahisha.”​—James, 17.

  •   Inaweza kukusababishia matatizo​—hasa ikiwa unataka sana kujiunga na kikundi fulani bila kujali wanataka ufanye nini.

     “Kinachotokea ni kwamba mtu mmoja tu mbaya katika kikundi cha marafiki anaweza kushawishi kikundi chote kifanye jambo baya.”​—Martina, 17.

 Unaweza kufanya nini?

  •   Chunguza viwango vyako.

     Jiulize hivi: ‘Ni viwango gani ninavyojitahidi kuvifuata? Je, marafiki wangu wanafanya iwe rahisi au vigumu kwangu kufuata viwango hivyo? Je, nitashikamana na marafiki hao haidhuru wanataka nifanye nini?’

     Kanuni ya Biblia: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”​—1 Wakorintho 15:33.

     “Unaposhirikiana na kikundi cha watu ambao viwango vyenu havifanani, unaweza kujikuta ukifanya mambo ambayo hungependa kuyafanya.”​—Ellen, 14.

  •   Chunguza mambo unayotanguliza.

     Jiulize hivi: ‘Je, ninakipenda sana kikundi changu cha marafiki hivi kwamba niko tayari kulegeza viwango vyangu ili nikubalike? Ninaweza kufanya nini rafiki yangu akifanya jambo fulani baya?’

     Kanuni ya Biblia: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia.”​—Ufunuo 3:​19.

     “Ikiwa mtu mmoja katika kikundi amefanya jambo fulani baya na mnahitaji kuwa washikamanifu kwake licha ya hali hiyo, unaweza kuonekana kama msaliti ukikemea jambo hilo.”​—Melanie, 22.

  •   Tafuta marafiki wengine.

     Jiulize hivi: ‘Je, ninaweza kufaidika nikiongeza idadi ya marafiki ili kutia ndani baadhi ya watu ambao siwajui vizuri?’

     Kanuni ya Biblia: ‘Endeleeni kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’​—Wafilipi 2:4.

     “Watoto ambao mara nyingi hupuuzwa wanaweza kuwa wanastahimili hali fulani ngumu nyumbani. Unapokuja kuwajua vizuri, ndipo unapotambua wana sifa zenye kupendeza ambazo hazionekani wazi.”​—Brian, 19.

 Jambo kuu: Hakuna ubaya wa kuwa na kikundi cha marafiki wa karibu. Wakati huohuo unaweza kunufaika kwa kuongeza idadi ya marafiki wapya tofauti na wale uliowazoea. Biblia inasema hivi: “Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”​—Methali 11:25.