Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Urafiki wa Kimapenzi—Sehemu ya 1: Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

Urafiki wa Kimapenzi—Sehemu ya 1: Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

Urafiki wa kimapenzi ni nini?

  Watu wengine huona urafiki wa kimapenzi kuwa jambo la kujifurahisha tu. Hata hivyo, katika makala hii, “urafiki wa kimapenzi” ni kipindi ambacho watu wawili wa jinsia tofauti hutumia muda pamoja ili kuona kama watafaana katika ndoa. Kwa hiyo, urafiki wa kimapenzi una kusudi. Si njia tu ya kufurahia kutendewa vizuri au kushirikiana kwa ukaribu na mtu wa jinsia tofauti.

 Urafiki wa kimapenzi unapaswa kukusaidia kufikia uamuzi—uamuzi wa kufunga ndoa na mtu uliyeanzisha urafiki naye au uamuzi wa kukomesha urafiki huo. Unapoanzisha urafiki wa kimapenzi unapaswa kuelewa kwamba urafiki huo unaweza kuongoza kwenye ndoa au unaweza kuvunjika.

 Jambo kuu: Ikiwa unahisi uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi basi unapaswa kuwa tayari pia kufunga ndoa.

Kuanzisha urafiki wa kimapenzi bila lengo la kufunga ndoa ni kama kwenda kwenye mahojiano ya kuomba kazi bila lengo la kupata ajira

Je, uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi?

  Kwa kuwa lengo la urafiki wa kimapenzi ni kufunga ndoa, ni muhimu sana kuchunguza sifa zako kwa sababu zinaweza kuchangia furaha au huzuni katika ndoa. Kwa mfano, fikiria mambo yafuatayo:

  •   Uhusiano wako na wengine katika familia. Jinsi unavyowatendea wazazi wako na ndugu na dada zako—hasa unapokuwa na mkazo—ni ishara ya jinsi utakavyomtendea mwenzi wako.

     Kanuni ya Biblia: “Acheni kabisa kila aina ya chuki yenye uhasama, hasira, ghadhabu, kufoka, matusi, na mambo yote yanayodhuru.”​—Waefeso 4:31.

     Jiulize: ‘Je, wazazi wangu na ndugu na dada zangu wanaweza kusema kwamba mimi huwatendea kwa heshima? Kutoelewana kunapotokea kati yangu na mmoja wao, je, mimi huzungumza kwa utulivu, au ninakasirika na kuanza mabishano?’

    Ikiwa unashindwa kushughulikia hali ya kutoelewana kati yako na wazazi wako, je, kweli utaweza kushughulikia hali kama hiyo ikitokea kati yako na mwenzi wako?

  •   Kujidhabihu. Utakapofunga ndoa, utahitaji kumfikiria mwenzi wako na wakati mwingine kudhabihu mapendezi yako ili kufanya mambo anayopendelea.

     Kanuni ya Biblia: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”​—1 Wakorintho 10:24.

     Jiulize: ‘Je, sikuzote mimi husisitiza mambo yafanywe vile ninavyotaka? Je, wengine wanaweza kusema kwamba mimi nina usawaziko? Nimeonyesha katika njia zipi kwamba ninatanguliza mahitaji ya wengine?’

  •   Unyenyekevu. Mwenzi wa ndoa anayefaa hukubali makosa yake na kuomba msamaha kutoka moyoni.

     Kanuni ya Biblia: “Sisi sote hufanya makosa mara nyingi.”​—Yakobo 3:2, maelezo ya chini.

     Jiulize: ‘Je, mimi huwa tayari kukubali makosa yangu au ninapenda kujitetea? Je, mimi hukasirika watu wanaponipa ushauri unaoweza kunisaidia?’

  •   Pesa. Mtu anayetumia pesa vizuri ataepuka tatizo linalofanya watu wakosane sana katika ndoa.

     Kanuni ya Biblia: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?”​—Luka 14:28.

     Jiulize: ‘Je, ninaweza kudhibiti kiasi cha pesa ninachotumia, au mara nyingi ninajipata nikiwa na madeni? Nimeonyeshaje kwamba ninaweza kutumia pesa kwa busara?’

  •   Ratiba ya kiroho. Ikiwa wewe ni Shahidi wa Yehova, unapaswa kuwa na ratiba nzuri ya kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

     Kanuni ya Biblia: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”​—Mathayo 5:3.

     Jiulize: ‘Je, mimi hufanya jitihada za kibinafsi ili kuimarisha imani yangu? Je, mimi hutanguliza ratiba yangu ya kiroho, au ninaacha mambo mengine yaivuruge?’

 Jambo kuu: Mtu utakayefunga ndoa naye anastahili mwenzi anayefaa. Ikiwa unajitahidi kuwa mtu anayefaa, inaelekea itakuwa rahisi zaidi kwako kupata mwenzi anayefanya jitihada kama zako.