Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 1: Ichunguze Biblia Yako

Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 1: Ichunguze Biblia Yako

 “Nimejaribu kuisoma Biblia, lakini kila wakati ninashindwa kwa sababu ni kubwa sana!”​—Briana.

 Je, wewe huhisi hivyo? Makala hii inaweza kukusaidia!

 Kwa nini nisome Biblia?

 Je, wazo la kusoma Biblia linakuchosha? Ikiwa ndivyo, inaeleweka. Huenda akilini mwako Biblia ni kitabu chenye maelfu ya kurasa yenye maandishi madogo-madogo na kisicho na picha yoyote. Kwa hiyo, ukiombwa uchague afadhali kutazama TV na video!

 Lakini fikiria hivi: Ukipata sanduku kubwa la zamani lenye hazina ndani, je, hungependa kujua ni nini kilicho ndani ya sanduku hilo?

 Biblia ni kama sanduku hilo la hazina. Ina vito vingi vya hekima ambavyo vitakusaidia

  •   Ufanye maamuzi mazuri

  •   Uwe na uhusiano mzuri na wazazi wako

  •   Upate marafiki wazuri

  •   Ukabiliane na mikazo

 Kitabu cha zamani hivyo kinawezaje kuwa na ushauri unaofaa hali zetu leo? Ni kwa sababu “kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:​16) Hilo linamaanisha kwamba ushauri wa Biblia umetoka kwenye Chanzo bora kabisa.

Biblia ni sanduku la hazina lililobeba hazina za hekima zenye thamani kubwa sana

 Ninaweza kuisoma Biblia jinsi gani?

 Njia moja ni kusoma Biblia kuanzia mwanzo hadi mwisho. Kufanya hivyo kutakupa picha ya ujumla ya ujumbe wa Biblia. Kuna njia nyingi za kusoma Biblia. Fikiria njia mbili:

  •    Unaweza kusoma vitabu vyote 66 vya Biblia kama vilivyopangwa, yaani, kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo.

  •    Unaweza kusoma kulingana na matukio ya Biblia, yaani, kulingana na jinsi matukio yalivyotokea.

 Dokezo: Nyongeza A7 katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ina mfululizo wa orodha ya matukio muhimu katika maisha ya Yesu duniani.

 Njia ya pili ya kusoma Biblia ni kuchagua simulizi linalopatana na changamoto unayokabili. Kwa mfano:

 Dokezo: Unaposoma Biblia, hakikisha upo kwenye mazingira matulivu ili uweze kukazia fikira usomaji wako.

 Njia ya tatu ya kusoma Biblia ni kuchagua simulizi au zaburi, uisome, na kisha ufikirie jinsi unavyoweza kutumia ulichosoma. Baada ya kusoma, jiulize maswali kama vile:

  •    Kwa nini Yehova aliongoza simulizi hili liandikwe?

  •    Simulizi hili linafunua nini kuhusu utu wa Yehova au njia yake ya kufanya mambo?

  •    Ninaweza kuitumiaje habari hii katika maisha yangu?

 Jiwekee malengo! Andika tarehe hususa ambayo ungependa kuanza programu ya usomaji wako wa Biblia kwa kutumia Ratiba ya Usomaji wa Biblia iliyo kwenye Tovuti yetu.