Mwanzo 49:1-33

  • Unabii wa Yakobo alipokuwa akifa (1-28)

    • Shilo atatoka Yuda (10)

  • Maagizo ya kumzika Yakobo (29-32)

  • Kifo cha Yakobo (33)

49  Basi Yakobo akawaita wanawe na kuwaambia: “Kusanyikeni pamoja niwaambie yatakayowapata katika kipindi cha mwisho cha zile siku.  Kusanyikeni msikilize, enyi wana wa Yakobo, naam, msikilizeni Israeli baba yenu.  “Rubeni,+ wewe ndiye mzaliwa wangu wa kwanza,+ nguvu zangu na mwanzo wa nguvu zangu za uzazi, ubora wa heshima na ubora wa nguvu.  Kwa vurugu kama maji yenye msukosuko, hutafanikiwa, kwa sababu ulikipanda kitanda cha baba yako.+ Wakati huo ulikichafua* kitanda changu. Kwa kweli alikipanda kitanda changu!  “Simeoni na Lawi ni ndugu.+ Silaha za ukatili ndizo silaha zao za kuchinjia.+  Usijiunge nao, Ee nafsi* yangu. Usijiunge na kusanyiko lao, Ee heshima yangu,* kwa sababu kwa hasira yao waliwaua wanaume,+ nao wakawakata ng’ombe dume mishipa ya miguu ili kujifurahisha.  Na ilaaniwe hasira yao, kwa sababu ni katili, na ghadhabu yao, kwa sababu ni kali.+ Acheni niwatawanye katika Yakobo, na acheni niwasambaze katika Israeli.+  “Nawe Yuda,+ ndugu zako watakusifu.+ Mkono wako utakuwa shingoni mwa maadui wako.+ Wana wa baba yako watainama chini mbele yako.+  Yuda ni mwanasimba.+ Mwanangu, kwa hakika utapanda juu kutoka mawindoni. Amejikunyata chini na kujinyoosha kama simba, na kama simba, ni nani anayethubutu kumwamsha? 10  Fimbo ya ufalme haitaondoka Yuda,+ wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo* atakapokuja,+ na mataifa yatamtii.+ 11  Atamfunga punda wake kwenye mzabibu na mwanapunda dume wake kwenye mzabibu bora, naye atafua nguo zake katika divai na vazi lake katika damu ya zabibu. 12  Macho yake ni mekundu sana kwa sababu ya divai, na meno yake ni meupe kwa sababu ya maziwa. 13  “Zabuloni+ atakaa kwenye ufuo wa bahari, kwenye ufuo ambapo meli hutia nanga,+ na mpaka wake wa mbali utaelekea Sidoni.+ 14  “Isakari+ ni punda mwenye mifupa migumu, aliyelala chini kati ya mizigo miwili aliyobeba. 15  Naye ataona kwamba mahali pa kupumzikia ni pazuri na kwamba nchi inapendeza. Atainamisha bega lake ili abebe mzigo, naye atakubali kufanya kazi ya utumwa. 16  “Dani+ atawahukumu watu wake akiwa mmoja wa makabila ya Israeli.+ 17  Dani na awe nyoka kando ya barabara, nyoka mwenye pembe kando ya njia, anayeuma visigino vya farasi na kumwangusha nyuma mpandaji wake.+ 18  Nitasubiri wokovu kutoka kwako, Ee Yehova. 19  “Naye Gadi+ atavamiwa na kundi la wavamizi, lakini atawavamia kwenye visigino vyao.+ 20  “Mkate wa Asheri+ utakuwa mwingi sana,* naye ataandaa chakula kinachomfaa mfalme.+ 21  “Naftali+ ni paa jike mwembamba. Anasema maneno yanayovutia sana.+ 22  “Yosefu+ ni chipukizi la mti unaozaa matunda mengi, mti ulio kando ya chemchemi unaozaa matunda mengi, wenye matawi yanayoenea juu ya ukuta. 23  Lakini wapiga mishale waliendelea kumshambulia na kumpiga kwa mishale na kuendelea kuwa na uadui dhidi yake.+ 24  Lakini bado upinde wake ulibaki mahali pake,+ na mikono yake ikaendelea kuwa na nguvu na myepesi.+ Alitiwa nguvu na mikono ya mwenye nguvu wa Yakobo, mchungaji, jiwe la Israeli. 25  Anatoka* kwa Mungu wa baba yako, naye atakusaidia, naye yuko pamoja na Mweza-Yote, atakubariki kwa baraka za mbingu zilizo juu, kwa baraka za vilindi vilivyo chini,+ kwa baraka za matiti na tumbo la uzazi. 26  Baraka za baba yako zitakuwa bora kuliko baraka za milima ya milele, bora kuliko vitu vyenye kutamanika vya vilima vinavyodumu.+ Zitaendelea kuwa juu ya kichwa cha Yosefu, juu ya utosi wa kichwa cha yule aliyechaguliwa kutoka kati ya ndugu zake.+ 27  “Benjamini+ ataendelea kurarua kama mbwamwitu.+ Asubuhi atakula mawindo, na jioni atagawanya nyara.”+ 28  Hayo yote ndiyo makabila 12 ya Israeli, na hivyo ndivyo baba yao alivyowaambia alipokuwa akiwabariki. Alimpa kila mmoja wao baraka inayomfaa.+ 29  Baada ya hayo aliwapa maagizo haya: “Nakaribia kufa.*+ Nizikeni pamoja na baba zangu katika pango lililo kwenye shamba la Efroni Mhiti,+ 30  pango lililo katika shamba la Makpela mbele ya Mamre katika nchi ya Kanaani, shamba ambalo Abrahamu alinunua kutoka kwa Efroni Mhiti ili liwe mahali pa kuzikia. 31  Walimzika huko Abrahamu na Sara mke wake.+ Walimzika huko Isaka+ na Rebeka mke wake, na huko ndiko nilikomzika Lea. 32  Shamba hilo na pango lililomo lilinunuliwa kutoka kwa wana wa Hethi.”+ 33  Basi Yakobo akamaliza kuwapa wanawe maagizo hayo. Kisha akairudisha miguu yake kitandani, akakata pumzi, naye akazikwa pamoja na watu wake.*+

Maelezo ya Chini

Au “ulikitia unajisi.”
Angalia Kamusi.
Au labda, “mtazamo wangu.”
Maana yake “Yule Ambaye Ni Yake; Yule Ambaye Ni Mali Yake.”
Au “Chakula cha Asheri kitakuwa kingi sana.”
Yaani, Yosefu.
Tnn., “Nakusanywa kwa watu wangu.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.