Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutatua Matatizo

Kutatua Matatizo

Siri ya Furaha ya Familia

Kutatua Matatizo

Mume anauliza: “Mabinti wetu wako wapi?”

Mke anajibu: “Wameenda madukani kununua nguo mpya.”

Mume anasema: [Kwa sauti kubwa huku akiwa amekasirika] “Eti wameenda kununua ‘nguo mpya’? Lakini walinunua nguo mpya mwezi uliopita!”

Mke anajibu: [Anajitetea, akihisi uchungu moyoni kwa kuwa mume wake anamlaumu] “Lakini kuna nguo zinazopigwa mnada. Na waliniomba ruhusa kwanza, nami nikawaruhusu waende.”

Mume anasema: [Akiwa amekasirika sana na kuongea kwa sauti ya juu] “Unajua kwamba sipendi mabinti wetu watumie pesa bila kuniomba ruhusa! Kwa nini uliamua hivyo haraka-haraka bila kuniambia?”

UNAFIKIRI wenzi hao wa ndoa wanahitaji kutatua matatizo gani? Ni wazi kwamba mume anashindwa kuzuia hasira yake. Hata hivyo, inaonekana kwamba wenzi hao hawaelewani kuhusu uhuru ambao wanapaswa kuwapa watoto wao. Na inaonekana kwamba kuna tatizo la mawasiliano.

Hakuna ndoa ambayo ni kamilifu. Ndoa zote zinakabili matatizo fulani. Mume na mke wanapaswa kujifunza kusuluhisha matatizo yao, yawe makubwa au madogo. Kwa nini?

Baada ya muda, matatizo yasiyosuluhishwa yanaweza kuwa kama ukuta unaozuia mawasiliano. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Kuna magomvi yaliyo kama pingo la mnara wa makao.” (Methali 18:19) Unaweza kufanya nini ili kuboresha mawasiliano unaposhughulikia matatizo?

Mawasiliano katika ndoa ni kama damu ya uhai mwilini, na upendo na heshima ni kama moyo na mapafu yanayosukuma damu hiyo. (Waefeso 5:33) Inapohusu kusuluhisha matatizo, upendo utawachochea wenzi wa ndoa kusahau makosa na maumivu ya kihisia ya wakati uliopita, na kukazia fikira tatizo wanalokabili sasa. (1 Wakorintho 13:4, 5; 1 Petro 4:8) Wenzi ambao wanaonyesha heshima wanawaruhusu wenzi wao waongee kwa uhuru na kujitahidi kuelewa yale yanayosemwa badala ya kusikiliza tu.

Hatua Nne za Kusuluhisha Matatizo

Fikiria hatua nne zilizoonyeshwa hapa chini, na uone jinsi kanuni za Biblia zinavyoweza kukusaidia kusuluhisha matatizo kwa njia ya upendo na heshima.

1. Pangeni wakati wa kuzungumzia tatizo. “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, . . . wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:1, 7) Kama kisa kilichosimuliwa mwanzoni kilivyoonyesha, matatizo fulani yanaweza kufanya hasira ipande. Hilo likitokea, jizuie na usimamishe mazungumzo kwa muda—‘kaa kimya’—kabla hasira haijawaka. Unaweza kuzuia uhusiano wenu usiharibike ukitii shauri hili la Biblia: “Kuanzisha ugomvi ni kama kufanya ufa kwenye bwawa; achana na ugomvi kabla haujafurika.”—Methali 17:14, Biblia Habari Njema.

Hata hivyo, pia kuna “wakati wa kusema.” Matatizo ni kama magugu ambayo yanasitawi yakiachiliwa. Basi usipuuze tatizo, ukifikiri kwamba litakwisha tu. Ukikatiza mazungumzo, mwonyeshe mwenzi wako wa ndoa heshima kwa kuchagua wakati wa kuzungumzia tatizo hilo bila kukawia. Ahadi kama hiyo inaweza kuwasaidia nyote wawili kufuata kanuni hii ya Biblia: “Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Bila shaka, unahitaji kutimiza ahadi yako.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Pangeni wakati fulani hususa kila juma wa kuzungumzia matatizo ya familia. Mkigundua kwamba kwa kawaida kuna wakati fulani ambapo mnabishana—labda, mnapofika nyumbani kutoka kazini au kabla ya kula—mkubaliane kutozungumzia matatizo nyakati hizo. Badala yake, chagueni wakati ambapo inaelekea nyote wawili hamtakuwa na mkazo mwingi.

2. Eleza maoni yako kwa unyoofu na kwa heshima. “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) Ikiwa umefunga ndoa, basi jirani yako wa karibu zaidi ni mwenzi wako wa ndoa. Kwa hivyo, mwambie mwenzi wako hisia zako waziwazi na kwa unyoofu. Margareta, * ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 26, anasema hivi: “Baada tu ya kuolewa, nilimtazamia mume wangu ajue jinsi nilivyohisi tatizo lilipotokea. Nilijifunza kwamba hilo halikuwa jambo linalofaa. Sasa ninajitahidi kumweleza hisia na maoni yangu waziwazi.”

Kumbuka kwamba kusudi lako mnapozungumzia tatizo si kushinda vita au kumshinda adui, badala yake ni kumruhusu mwenzi wako ajue maoni yako. Njia nzuri ya kufanya hivyo ni kufafanua tatizo ni nini, kusema linatokea wakati gani, kisha ueleze jinsi unavyohisi kulihusu. Kwa mfano, ikiwa unakasirika kwa sababu mwenzi wako anachafua nyumba, unaweza kusema hivi kwa heshima: ‘Unaporudi nyumbani kutoka kazini na kuacha nguo zako sakafuni [kutaja tatizo ni nini na wakati linapotokea], ninahisi kwamba huthamini jitihada zangu za kutunza nyumba [kueleza waziwazi jinsi unavyohisi].’ Kisha, pendekeza kwa busara suluhisho la tatizo hilo.

JARIBU KUFANYA HIVI: Ili uweze kukumbuka vizuri mambo unayotaka kuzungumza na mwenzi wako, andika maoni yako kuhusu tatizo na jinsi ambavyo ungependa lisuluhishwe.

3. Sikiliza na uelewe hisia za mwenzi wako. Mwanafunzi Yakobo aliandika kwamba Wakristo wanapaswa kuwa ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema, na si wepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Kuhisi kwamba mwenzi wako haelewi jinsi unavyohisi kuhusu tatizo fulani ni kati ya mambo machache yanayoumiza sana katika ndoa. Kwa hivyo, azimia kutomfanya mwenzi wako ahisi hivyo!—Mathayo 7:12.

Wolfgang, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 35, anasema hivi: “Tunapozungumzia matatizo, ninakuwa na wasiwasi moyoni, hasa ninapohisi kwamba mke wangu haelewi njia yangu ya kufikiri.” Dianna, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 20 sasa, anasema, “Mara nyingi ninamlalamikia mume wangu kwamba hanisikilizi kamwe tunapozungumzia matatizo.” Unaweza kutatua tatizo hilo jinsi gani?

Usikate kauli kwamba unajua hisia au maoni ya mwenzi wako wa ndoa. Neno la Mungu linasema hivi: “Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Mheshimu mwenzi wako kwa kumpa nafasi ya kueleza maoni yake bila kumkatiza. Kisha, ili kuhakikisha kwamba umeelewa mambo ambayo mwenzi wako amesema, mweleze kwa maneno yako yale ambayo amesema, bila kukasirika wala kumdhihaki. Mruhusu mwenzi wako akusahihishe ikiwa hukuelewa jambo fulani alilosema. Usizungumze tu bila kumpa mwenzi wako nafasi ya kueleza jinsi anavyohisi. Tumieni njia hiyo ya mawasiliano mpaka nyote wawili mkubaliane kwamba kila mmoja ameelewa maoni na hisia za mwenzi wake kuhusu tatizo hilo.

Ni kweli kwamba unahitaji unyenyekevu na subira ili umsikilize mwenzi wako kwa makini na kukubali maoni yake. Lakini ikiwa utachukua hatua ya kwanza kumheshimu mwenzi wako wa ndoa, itakuwa rahisi zaidi kwake kukuheshimu.—Mathayo 7:2; Waroma 12:10.

JARIBU KUFANYA HIVI: Unaporudia mambo ambayo mwenzi wako amesema, usirudie tu maneno yaleyale aliyosema. Kwa huruma, jaribu kueleza jinsi unavyoelewa hisia na maoni ya mwenzi wako.—1 Petro 3:8.

4. Mkubaliane kuhusu suluhisho. “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.” (Mhubiri 4:9, 10) Wenzi wa ndoa wasiposhirikiana na kutegemezana, hawawezi kusuluhisha matatizo mengi ya ndoa.

Ni kweli kwamba Yehova alimweka mume kuwa kichwa cha familia. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Lakini ukichwa si udikteta. Mume mwenye hekima hatafanya maamuzi bila kufikiria maoni ya mke wake. David, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 20, anasema, “Ninajitahidi kutafuta jambo ambalo linapatana na maoni ya mke wangu na kufanya uamuzi ambao sote tunaweza kuunga mkono.” Tanya, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka saba sasa, anasema hivi: “Hatutafuti ni nani mwenye kosa au asiye na kosa. Nyakati nyingine kuna maoni tofauti tu ya jinsi ya kusuluhisha tatizo. Nimegundua kwamba siri ya kufanikiwa ni kubadilika kulingana na hali na kuwa mwenye usawaziko.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Mnaweza kusitawisha roho ya ushirikiano kwa kuandika njia mbalimbali mnazoweza kutumia kusuluhisha tatizo. Baada ya kuandika njia zote mnazofikiria, pitieni orodha yenu na kuchagua suluhisho ambalo nyote wawili mnakubaliana nalo. Kisha pangeni wakati fulani baadaye ili mchunguze ikiwa mlitekeleza uamuzi huo na mmefanikiwa kadiri gani.

Fanyeni Kazi Pamoja, Msitengane

Yesu alifananisha ndoa na nira. (Mathayo 19:6) Katika siku za Yesu, nira ilikuwa ubao ambao ulifunga wanyama wawili pamoja ili wafanye kazi. Ikiwa wanyama hao hawangeshirikiana, hawangefanya kazi vizuri na nira hiyo ingewaumiza shingoni. Wanyama waliofanya kazi pamoja, waliweza kuvuta mizigo mizito au kulima shamba.

Vivyo hivyo, mume na mke ambao hawawezi kufanya kazi pamoja kwa ushirikiano wanaweza kuumia chini ya nira ya ndoa. Kwa upande mwingine, wakijifunza kufanya kazi pamoja, wanaweza kusuluhisha karibu matatizo yote na kutimiza mambo mengi. Mume fulani mwenye ndoa yenye furaha anayeitwa Kalala anasema hivi kwa ufupi: “Kwa miaka 25, mimi na mke wangu tumesuluhisha matatizo yetu kwa kuzungumza kwa uhuru na unyoofu, kufikiria hisia za mwingine, kusali ili Yehova atusaidie, na kutumia kanuni za Biblia.” Je, mnaweza kufanya hivyo?

JIULIZE . . .

▪ Ni tatizo gani ambalo ninataka sana kuzungumzia pamoja na mwenzi wangu wa ndoa?

▪ Ninaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba ninaelewa kabisa hisia za mwenzi wangu kuhusu jambo hili?

▪ Ni matatizo gani yanayoweza kutokea ikiwa nyakati zote ninasisitiza kufanya mambo kwa njia yangu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Baadhi ya majina yamebadilishwa.