Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Faida za Kuwa Mkarimu

Furahia Faida za Kuwa Mkarimu

“BASI linaweza kuondoka, lakini Mchina huyu atabaki!” Mwanamke mmoja anayeitwa Alexandra alisikia maneno hayo alipokuwa kwenye basi akingojea kuvuka mpaka kati ya nchi mbili za Amerika ya Kusini. Aliposhuka alimkuta kijana Mchina akijaribu kujieleza kwa Kifaransa ambacho hakukijua vizuri, kuhusu matatizo yake kwa askari wa mpakani. Kwa kuwa Alexandra anahudhuria ibada katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Kichina, alijitolea kuwa mkalimani.

Mwanaume huyo alikiri kwamba yeye ni raia halali, lakini, alikuwa ameibiwa pesa na vitambulisho vyake. Mwanzoni askari huyo hakuamini jambo hilo, hata alidhani kwamba Alexandra anafanya biashara haramu ya kusafirisha watu kwa njia ya magendo. Hatimaye, askari huyo alikubali maelezo ya mwanaume huyo, lakini alimpiga faini kwa kukosa kuwa na vitambulisho vinavyofaa. Kwa kuwa mwanaume huyo hakuwa na pesa, Alexandra alijitolea kumwazima dola 20. Mwanaume huyo alimshukuru sana na aliahidi atamlipa zaidi ya dola 20. Alexandra alimweleza kuwa lengo lake si kupata faida; bali alifurahi kumsaidia kwa kuwa alihisi kufanya hivyo ni jambo linalofaa. Kisha, alimpatia baadhi ya machapisho ya Biblia na kumtia moyo ajifunze na Mashahidi.

Inatia moyo kusikia watu wakiwaonyesha wageni ukarimu, bila shaka, matendo kama hayo hufanywa na watu wa dini mbalimbali na hata wale wasio na dini. Je, ungekuwa tayari kujitoa mwenyewe bila ubinafsi kufanya hivyo? Ni muhimu kujiuliza swali hilo, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Pia, utafiti wa kisayansi unathibitisha kwamba kuwa mkarimu kuna faida nyingi kwako. Acheni tuone baadhi ya faida hizo.

“MTOAJI MCHANGAMFU”

Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba kuna uhusiano wa karibu kati ya kutoa na kuwa na furaha. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” Mtume huyo alikuwa akizungumzia kuhusu Wakristo ambao walitoa michango kwa ukarimu kuwasaidia waamini wenzao waliokuwa na uhitaji. (2 Wakorintho 8:4; 9:7) Paulo hakusema kwamba walitoa kwa sababu walikuwa wenye furaha. Kinyume chake ni kwamba, walikuwa na furaha kwa sababu walitoa.

Kwa kweli, kulingana na utafiti mmoja, kutoa “kunachochea utendaji katika sehemu fulani ya ubongo inayohusiana na furaha, uhusiano wa kijamii, tumaini, hivyo kufanya mtoaji ‘ajihisi vizuri.’” Utafiti mwingine unaonyesha kuwa “kumpa mtu mwingine pesa huchangia furaha ya mtu anayetoa, ukilinganisha na jinsi angehisi ikiwa angezitumia mwenyewe.”

Je, umewahi kuhisi kwamba hali zako hazikuruhusu kufanya mengi? Ukweli ni kwamba kila mtu anaweza kupata shangwe ya kuwa “mtoaji mchangamfu.” Hata iwe tunatoa kitu chenye thamani ndogo, kutoa kwa nia nzuri kunatimiza jambo muhimu sana. Shahidi wa Yehova mmoja aliwatumia wachapishaji wa gazeti hili, mchango na ujumbe uliosema hivi: “Kwa miaka yote hii sikuweza kuchangia mchango mkubwa isipokuwa kiasi kidogo tu katika Jumba la Ufalme.” Lakini aliongezea hivi: “Yehova Mungu amenipa vingi zaidi kuliko nilivyotoa. . . . Asanteni kwa kufanya iwezekane kutoa zawadi hii, jambo hili limenifariji.”

Bila shaka, kutoa hakuhusishi pesa pekee. Kuna njia mbalimbali za kutoa.

KUTOA KUNA FAIDA KWA AFYA YAKO

Kuwa mkarimu kuna faida kwako na kwa wengine

Biblia inasema hivi: “Mwanamume mwenye fadhili zenye upendo anaitendea kwa kuipa thawabu nafsi yake mwenyewe, lakini mtu mkatili anajiletea taabu.” (Methali 11:17) Mtu mwenye fadhili ni mkarimu na yuko tayari kujitoa, yaani, kutumia muda, nguvu, na kadhalika ili kuwahudumia wengine. Mtu anayefanya mambo hayo hufaidika kwa njia mbalimbali, na zaidi ya yote ni kwamba ukarimu huchangia kuwa na afya nzuri.

Utafiti unaonyesha kwamba watu wanaojitolea kuwasaidia wengine, hawashuki moyo au kuugua mara nyingi. Zaidi ya yote, wanafurahia kuwa na afya nzuri. Kutoa kwa ukarimu kunaboresha afya ya watu wanaougua baadhi ya magonjwa mbalimbali, kama vile ugonjwa wa mfumo wa neva au HIV. Pia, imeonekana kwamba mtu anayepambana kushinda uraibu wa pombe, anapowasaidia wengine jambo hilo humwezesha kushinda tamaa ya kurudia zoea lake na kutoshuka moyo sana.

Jambo hilo linawezekana kwa sababu inaelezwa kwamba “kuonyesha huruma, wema, na fadhili huzuia mtu kuwa na hisia mbaya.” Pia, kutoa kunapunguza mkazo na shinikizo la damu. Hata watu waliofiwa na wenzi wao hupona haraka dalili za kushuka moyo wanapojitolea kuwasaidia wengine.

Hakuna shaka kwamba kutoa kutakuletea faida nyingi sana.

UKARIMU HUCHOCHEA WENGINE WAWE WAKARIMU

Yesu aliwahimiza wafuasi wake kwa kusema hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.” (Luka 6:38) Unapotoa kwa ukarimu, inaelekea watu watakushukuru na wao pia wataonyesha ukarimu. Hivyo, kutoa huchochea ushirikiano na urafiki.

Kutoa huchochea ushirikiano na urafiki

Watafiti wanaochunguza mahusiano ya wanadamu wamegundua kwamba “watu wanaojitolea kwa hiari huwachochea wengine kufanya vivyohivyo.” Kwa kweli, “hata kusoma tu kuhusu matendo ya fadhili huwachochea watu kuwa wakarimu zaidi.” Hivyo, kulingana na utafiti mmoja, “kila mtu katika mtandao anaweza kuchochea mamia au maelfu ya watu, hata wale ambao hawamjui au hawajawahi kuonana naye.” Kwa maneno mengine ni kwamba, tendo moja la ukarimu ni kama wimbi dogo linaloanza na kuenea kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine mpaka kufikia jamii yote. Je, ungependa kuishi kwenye jamii kama hiyo? Naam, bila shaka tungepata faida nyingi ikiwa watu wote wangekuwa wakarimu.

Tukio moja linaonyesha matokeo mazuri ya ukarimu lilitokea Florida, nchini Marekani. Kikundi cha Mashahidi wa Yehova kilijitolea kutoa misaada baada ya eneo hilo kukumbwa na dhoruba. Walipokuwa wanangojea vifaa katika nyumba ambayo walikuwa wanarekebisha, Mashahidi hao waliona wigo wa nyumba ya jirani uliokuwa umebomoka, nao wakajitolea kuurekebisha. Baadaye jirani huyo aliandika barua kwa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova iliyosema hivi: “Nitawashukuru daima,” kisha, akaongeza: “Sijawahi kukutana na watu wazuri kama hawa.” Kwa kuchochewa na moyo wa shukrani ulituma mchango wake utumiwe kwa ajili ya kazi ya pekee ya Mashahidi.

MWIGE MTOAJI MKUU

Utafiti wa kisayansi unaonyesha kwamba “kimsingi kuwasaidia wengine ni mwelekeo wa asili wa wanadamu.” Utafiti huo unasema kwamba, “watoto wana uwezo wa kuonyesha sifa ya ukarimu hata kabla ya kujifunza kuongea.” Kwa nini? Biblia inatoa jibu inaposema kuwa wanadamu waliumbwa kwa “mfano wa Mungu,” na hilo linamaanisha kwamba wana uwezo wa kuonyesha sifa kama za Mungu.—Mwanzo 1:27.

Miongoni mwa sifa zenye kuvutia sana za Muumba wetu, Yehova Mungu ni ukarimu. Ametupatia uhai na vitu vyote vinavyofanya tuwe na furaha. (Matendo 14:17; 17:26-28) Tunaweza kumjua Baba yetu wa mbinguni na makusudi yake yenye upendo kwa kujifunza Neno lake Biblia. Kitabu hicho kinaeleza kwamba Mungu ameandaa wakati ujao ulio mzuri ili tuwe na furaha. * (1 Yohana 4:9, 10) Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye chanzo cha ukarimu, na tumeumbwa kwa mfano wake, haishangazi kwamba kumwiga Mungu kwa kuwa mkarimu, kuna faida kwako na kutakuwezesha kupata kibali chake.—Waebrania 13:16.

Je, unamkumbuka Alexandra, aliyetajwa mwanzo mwa makala hii? Ukarimu wake ulikuwa na matokeo gani? Ingawa abiria wengine walisema kwamba ametupa pesa zake, mwanaume aliyesaidiwa aliwasiliana na rafiki zake walio katika jiji jingine ambapo basi hilo lilisimama, na akalipa haraka lile deni la dola 20. Zaidi ya hayo, mwanaume huyo alifuata ushauri wa Alexandra na kuanza kujifunza Biblia. Alexandra alifurahi kuonana tena na mwanaume huyo miezi mitatu baadaye katika kusanyiko la lugha ya Kichina la Mashahidi wa Yehova lililofanyika nchini Peru. Ili kumshukuru kwa wema wote aliomfanyia, mwanaume huyo alimwalika Alexandra na wote waliosafiri naye kwenye mkahawa wake kwa ajili ya chakula.

Kutoa na kuwasaidia wengine huleta shangwe nyingi. Zaidi ya yote, ni njia ambayo unaweza kuwasaidia wengine wamjue vizuri yule aliye Chanzo cha kila zawadi njema, Yehova Mungu! (Yakobo 1:17) Je, unafurahia faida za kuwa mkarimu?

^ fu. 21 Ili kupata habari zaidi, soma kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na pia kinapatikana kwenye www.mr1310.com/sw. Tafuta kwenye MACHAPISHO > VITABU NA BROSHUA.